Home 2023 January 15 JE! TWAJITAABISHA BURE?

JE! TWAJITAABISHA BURE?

JE! TWAJITAABISHA BURE?

“Basi, ndugu zangu wapendwa, mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.” (1 Wakorintho 15:58)

Maneno yenye utukufu yanayoleta uhakikisho!

Je! Ni nani kati yetu ambaye hajawahi kuhisi, wakati mmoja au mwingine, kwamba kazi yetu kwa Bwana ikaonekana kama ni bure? Katika nyakati kama hizo, ni faraja iliyoje kupumzika katika uhakikisho huu usio na masharti, uliotolewa na Mungu wetu kwamba kazi yetu kwa ajili Yake; kwa ajili ya Jina Lake, siyo kazi bure!

Lakini je! Mtume Paulo aliwezaje kusema jambo kama hilo, kulingana na maneno yake kwa Wagalatia? Kwa hao, alisema:

“Nawachelea, isiwe labda nimejitaabisha bure kwa ajili yenu” (Wagalatia 4:11)

Katika Kifungu hicho Mtume Paulo anaonekana kuogopa kwamba kazi yake ya ‘kuwakalisha’ Wagalatia katika fundisho la neema ya Mungu ingekuwa bure kama wangeendelea kuitamani Sheria!

Na je! Vipi kuhusu Wafilipi 2:16; Ambapo Mtume Paulo anawahimiza Wafilipi kuwa:

“Mkishika neno la uzima; nipate sababu ya kuona fahari katika siku ya Kristo, ya kuwa sikupiga mbio bure wala sikujitaabisha bure.”

Hapa inaonekana kana kwamba kazi ya Mtume Paulo ingekuwa ni ya bure ikiwa Wafilipi wangeshindwa kushikilia neno la uzima, na kufuata maagizo yake mengine.

Kama hayo hayatoshi, kuna pia 1 Wathesalonike 3:5 ambayo inatupasa pia kuizingatia, ambapo Paulo aliwaambia Wathesalonike,

“Kwa hiyo mimi nami nilipokuwa siwezi kuvumilia tena, nalituma mtu ili niijue imani yenu, asije yule mjaribu akawajaribu, na taabu yetu ikawa haina faida.”

Hapa tena, Mtume Paulo anaonekana kuogopa kwamba kazi yote ambayo alikuwa ameifanya kwa watu wa Mungu inaweza kuwa bure ikiwa vishawishi vya mjaribu vingefaulu kuwavuta Wathesalonike waache imani.

Katika kuzizingatia kauli kama hizi, Mtume Paulo angewezaje kusema kwa ujasiri ule kwamba kazi ya Wakorintho haikuwa ya bure? Je! Wakorintho walifanya kazi nzuri na kubwa zaidi kuliko yeye? Hakika sivyo! Tunahisi jibu liko katika uhakikisho ambao Mtume Paulo aliwapa kwamba kazi yao haikuwa ya bure “katika Bwana.” Ingawa iliwezekana kwamba kazi ya hata mtume mkuu Paulo inaweza kuwa bure katika Wagalatia, katika Wafilipi, na katika Wathesalonike, lakini kamwe haiwezekani kwamba kazi yetu yoyote ikawa bure katika Bwana.

Ni kwanini hivyo? Vyema, kumbuka kile Mtume Paulo anakisema kuhusu Kiti cha Hukumu cha Kristo kwamba “kila mtu atapata thawabu yake mwenyewe sawasawa na taabu yake mwenyewe” (1 Wakorintho 3:8). Tambua kwamba tutalipwa kulingana na kazi yetu, na sio kulingana na matunda ya kazi yetu. Yaani, Mungu anakusudia kutupa thawabu kulingana na uaminifu wetu, na sio kulingana na uaminifu wa wale ambao ni ‘mazao’ ya kazi yetu. Kama isingekuwa hivyo, hata thawabu za Mtume Paulo zingekuwa chache, kwani baada ya kazi yote aliyoifanya katika Asia, wote walio wa Asia walimwepuka (2 Timotheo 1:15).

Ndio kusema, ikiwa ukosefu wa uaminifu wa wale ‘uliowazaa’ katika kazi yako ya kiroho inakufanya ufikiri kwamba jitihada zako zote zimeenda bure, kumbuka kwamba taabu zako zinaweza kuwa bure ndani yao, lakini taabu zako hizo hazikuwa bure katika Bwana. Unalo Neno la Mungu!

Bila shaka, kama hakutakuwa na Kiti cha Hukumu cha Kristo, basi kazi yako kwa ajili ya Bwana itakuwa ni bure hasa! Ikiwa wewe msomaji wa andiko hili utakuwa unashangaa kwa nini tunaweza kusema kitu kama hicho, kumbuka kwamba baadhi ya Wakorintho walikuwa wakisisitiza kwamba hakuna kitu kama ufufuo wa wafu (1 Wakorintho 15:12). Na kama hakuna ufufuo, hakutakuwa na Kiti cha Hukumu kitakachofuata, na kama hakutakuwa na Kiti cha Hukumu, basi kazi zetu zitakuwa ni bure! Mwendelezo huu wa mawazo haya yenye kasoro yalikuwa yanalenga (yanatishia) kusimamisha kazi yote kwa ajili ya Bwana katika Korintho! Si ajabu kwamba Mtume Paulo anaanza sura hii ya ufufuo kwa kwanza kuwahakikishia Wakorintho kwamba imani yao, katika Bwana, haikuwa “batili” (15:2,14,17), na kisha akaendelea kuwahakikishia kwamba kazi yao pia haikuwa “bure”.

Ingawa baadhi ya viongozi wengi wa kiroho, hasa nyakati hizi, huepuka kufundisha fundisho kwa sababu fundisho, katika fahamu zao, halitamaniki sana, lakini Mtume Paulo alikuwa na nia nyingine. Kutokuamini fundisho la ufufuo wa wafu kulikuwa kunatishia ‘kukamata’ imani na kazi ya watakatifu wa Korintho, lakini HOJA ambazo Mtume Paulo alizitoa kwa ajili ya fundisho la ufufuo katika sura hii iliyobarikiwa inaeleza kwa nini aliweza kusema tuwe na kichocheo chote tunachohitaji ili “tuzidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote.”

Na kwa hivyo, ikiwa wakati mwingine unahisi kama unazungusha gurudumu lako mahali pamoja na huendi popote na watu unapofanya nao kazi kwa ajili ya Bwana, tunahitimisha kwa ahadi nyingine isiyo na masharti kutoka kwa mtume wa neema:

“Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.” (Wagalatia 6:9)

UTUKUFU NA UWEZA UNA YEYE KRISTO YESU; AMINA.

Author: Festus Patta

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *