Home 2022 October 13 Kusudi la Umilele la Mungu

Kusudi la Umilele la Mungu

Kusudi la Umilele la Mungu

Je! Umewahi kuyafikiria kwa umakini maneno ya utangulizi ya Biblia? Biblia inajifungua kwa maneno haya:

“Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi” (Mwanzo 1:1)

Je! Ni kwa nini Biblia haianzi tu kwa kusema kwamba “Hapo mwanzo Mungu aliumba Ulimwengu”? Kwa nini mbingu na nchi?

Tunapoendelea kuisoma Biblia yetu kwa umakini, tunapata jibu la swali hilo, kwani Biblia inatufundisha wazi kabisa kwamba Mungu ana makusudi mawili katika uumbaji wake; moja linahusiana na ‘nchi’ na jingine na ‘mbingu’. Kusudi la kwanza ni habari ya UNABII, wakati kusudi la pili ni habari ya SIRI, iliyofunuliwa na kupitia kwa Mtume Paulo (angalia Matendo 3:21; na Warumi 16:25). Kusudi la kwanza linahusu Israeli na mataifa; na kusudi la pili linahusu “Mwili wa Kristo”, Kanisa la mwito wa mbinguni.

Watu wengi wanashangaa wanapotambua kwamba, haiko ahadi hata moja katika Agano la Kale lote, inayohusu kwenda mbinguni! Katika agano hilo, mtazamo mzima ni wa kidunia, huku Masihi akitawala kama Mfalme (Yeremia 23:5; na penginepo). Wakati Bwana wetu alipojitokeza na kujidhihirisha katika mwili, malaika walishangiliza kwa kusema: “Na duniani iwe amani” (Luka 2:14b); na Yeye mwenyewe alisema kwamba “wenye upole, watairithi nchi” (Mathayo 5:5). Aliwafundisha wanafunzi Wake kusali hivi: “Mapenzi yako yafanyike duniani kama huko mbinguni” (Mathayo 6:10).

Hata kwenye ile siku ya Pentekoste, Mtume Petro alitangaza kwamba baada ya “kufanywa upya kwa vitu vyote” Mungu angemrudisha Yesu duniani na nyakati za kuburudishwa ‘zingekuja kwa kuwapo kwake Bwana’ (Matendo 3:19-21).

Ni mpaka wakati wa kuinuliwa kwa Mtume Paulo ulipowadia, ndipo tunapojifunza kwamba sasa waamini wote katika Kristo “wanabatizwa katika mwili mmoja” (1 Wakorintho 12:13), na Wakolosai 1:5 na vifungu vingine vingi vilivyoandikwa na Mtume Paulo, vinazungumza juu ya “tumaini lililowekwa kwa ajili yetu huko MBINGUNI”. Hakika, mbele za Mungu, waamini tayari wamepewa nafasi “katika ulimwengu wa roho” na wamebarikiwa kwa baraka zote za kiroho KATIKA [ULIMWENGU WA ROHO] katika Kristo (Waefeso 1:3; 2:4-7):

“Atukuzwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, aliyetubariki kwa baraka zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho, ndani yake Kristo.”

“Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema. Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu; ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu.”

Hata hivyo, unabii kuhusu Ufalme huo bado utatimizwa na Kristo atatawala duniani na kuleta “nyakati za kuburudishwa” zilizoahidiwa. Ni jambo la kumshukuru sana Mungu kwamba, ulimwengu huu hautakuwa daima, mahali pa vita na umwagaji damu, magonjwa na kifo, taabu na adha. Hakika, wakati huo ukifika, mbingu na nchi zitafunguliwa kwa kila kimoja kukielekea kingine, na hivyo litatimizwa kusudi la umilele la Mungu lenye sura mbili, kama Mtume Paulo alivyotuandikia:

“YAANI, KULETA MADARAKA YA WAKATI MKAMILIFU ATAVIJUMLISHA VITU VYOTE KATIKA KRISTO, VITU VYA MBINGUNI NA VITU VYA DUNIANI PIA. NAAM, KATIKA YEYE HUYO” (WAEFESO 1:10)

Author: Festus Patta

One Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *