Home 2022 August 22 WABEROYA WA KWELI!

WABEROYA WA KWELI!

WABEROYA WA KWELI!

Watu, vikundi, makundi, na mashirika mengi ya Kikristo yanajiita Waberoya, lakini inashangaza kuona wengi wao hawajui kabisa hata maana hasa ya Mberoya wa kweli kuwa ni nani!

Sura ya 17 ya Kitabu cha Matendo ya Mitume inatuelezea jinsi Paulo alivyowakusanya watu wa jamii yake (Wayahudi) huko Thesalonike na kwa siku tatu mfululizo za sabato “akahojiana nao kwa maneno ya maandiko,” akijaribu kuwaonyesha kwamba Yesu amhubiriye ndiye Kristo.

Hata hivyo, ndugu zake hao wakiwa ‘wamezama’ katika dini yao, wengi wao hawakutaka hata kuzitafakari zile kweli ambazo Paulo alikuwa akiwaeleza. Kimsingi, walichukizwa na ukweli kwamba baadhi yao walikiamini kile Paulo alichowaeleza; lakini wale walio wengi, kwa ushupavu mkubwa, ‘wakakutanisha makutano na wakafanya ghasia mjini’; kiasi kwamba maisha ya Paulo na Sila yakawa hatarini na hivyo ikawapelekea Wakristo wa huko, wawatorosha Paulo na Sila usiku na kuwapeleka hadi Beroya, mji uliokuwa kwenye umbali wa kama maili arobaini hivi.

Huko Beroya, Paulo aliwatafuta tena “watu wa jamii yake hiyo kwa jinsi ya mwili” – na huko akapata mapokezi tofauti na yale ya Thesalonike! Hivi ndivyo kumbukumbu za kimaandiko zinavyosema:

“Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo” (Matendo 17:11)

Watu hawa hawakufumba macho yao mara moja katika kupata mwanga zaidi. Badala yake, walimsikiliza Paulo kwa shauku, kwa akili iliyo wazi, kwa yale yote aliyokuwa akiyasema. Lakini pia, watu hawa hawakudanganyika kwa kuwa, baada ya kumsikiliza Paulo, walilitia lile neno lake kwenye MIZANI ya Neno la Mungu; wakayachunguza Maandiko kila siku ili waone kama mambo hayo ndivyo yalivyo. Kwa ajili ya hayo, Mungu aliwaita “waungwana”; kwa sababu walikuwa ni tabaka la kiungwana la kweli la kiroho la siku zao.

Sisi sote kwa hiyo, tunapaswa kuwa Waberoya, wakubwa vya kutosha katika roho; tunaoweza kusikiliza kwa akili iliyo wazi mafundisho ya wanadamu, na kisha kuwa na ukubwa wa kutosha kuyapima mafundisho yao kwenye MIZANI ya Neno la Mungu (Biblia), ili tuweze kujionea wenyewe kama kweli mambo hayo ndivyo yalivyo. Bwana wetu alisema: “Yachunguzeni Maandiko… kwa maana… yananishuhudia” (Yohana 5:39). Tunapofanya hivyo tunapata uzima wa milele – na zaidi – katika Kristo.

Utukufu una Yeye KRISTO, Milele na Milele; AMINA.

Author: Festus Patta

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *