Home 2022 July 30 Tuwe na Ujasiri

Tuwe na Ujasiri

Tuwe na Ujasiri

“Kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote;  pia na kwa ajili yangu mimi, nipewe usemi kwa kufumbua kinywa changu, ili niihubiri kwa ujasiri ile siri ya Injili; ambayo kwa ajili yake mimi ni mjumbe katika minyororo; hata nipate ujasiri katika huyo kunena jinsi inipasavyo kunena.” (Waefeso 6:18-20)

Katika siku zetu hizi za kisasa kuna mahitaji makubwa ya mafanikio ya kimwili, tena ya papo kwa hapo. Tunasoma mara kwa mara jinsi wengi walivyoinuka na kuwa maarufu kwa ‘bahati-bahati’ – kwa kipindi kifupi!

Hata hivyo, ni mara chache tunasikia kuhusu saa zao za kazi, mazoezi, dhabihu na nidhamu iliyowachukua ili kuyajenga ‘mafanikio’ hayo. Mara nyingi tumekuwa tunasikia na kuona tu matokeo ya mwisho. Wengi, kwa sababu hiyo, wamedanganyika na kudhani kwamba wanaweza kupata umaarufu huo na hivyo kuwa na mali nyingi ‘kimuujiza-ujiza’ bila ya kuwa na bidii yoyote ile katika chochote kile…

Ndiyo kusema, katika siku hizi tunazoishi, ‘ulimwengu’ unaonekana kuwa na ushawishi mkubwa na wenye nguvu juu ya maisha ya waumini wengi. Kwa sababu hii washirika wengi wa Mwili wa Kristo wanatafuta ‘kitabu’, ‘kongamano’, ‘semina’, ‘mtume’, ‘nabii’, ‘mchungaji’, ‘mwalimu’, mwinjilisiti’, ‘kanisa’, ‘dhehebu’, n.k.;  kama njia yake ya mkato ya ukomavu wa kiroho. Linapokuja suala la maisha yetu ya kiroho na suala la kuwa na ujasiri wa imani tunataka matokeo ya papo hapo kwa juhudi kidogo au bila kuwa na juhudi yoyote ile iliyowekwa ndani yake. Ili kuwa na ujasiri katika imani, kama Mtume Paulo alivyosema hapo juu, ni lazima kuwe na vitu vitatu muhimu.

Wakati

Kama vile ilivyo kwa ukuzi wa kimwili ambao huchukua miaka mingi, ukuzi wa kiroho pia huchukua muda. Kwa kadiri tunavyoufikia ukomavu wa kiroho, tunakuwa na ujasiri zaidi na zaidi wa kusema kwa ajili ya Bwana. Inachukua muda pia kutambua kwamba tunapaswa kuyaondoa macho yetu juu ya mambo yetu sisi wenyewe, jambo linalotufanya tuwe na wasiwasi wa kuzungumza kwa sababu ya hofu ya wanadamu.

Nidhamu

Kunahitajika nidhamu kukaa katika Neno la Mungu na kujifunza ili kupata ujuzi wa Maandiko. Hatumaanishi tu kusoma Biblia kwa sababu ya ‘ibada’. Inasemekana kwamba tunahifadhi takribani asilimia 20 tu ya yale tunayoyasoma. Lakini, ikiwa tunasoma na kujifunza, tunabakiwa na takribani asilimia 60 kwa kuyalinganisha Maandiko. Kwa kadiri unavyojitayarisha vyema katika Neno la Mungu, ndivyo utakavyokuwa na amani na ujasiri zaidi katika kulishuhudia Neno la Kweli, liligawanywa ipasavyo.

Uthabiti

Ikiwa tunataka kupata heshima kutoka kwa wengine katika kuihudumia injili kwa ufanisi, ni lazima tukubaliane na tuenende sambamba na ile KWELI. Tusipige ‘tarumbeta’ isiyo na hakika, tuweze kukithibitisha kile tunachokifundisha na Kitabu Kitakatifu. Sio tu kwamba tunapaswa kusema kweli mfululizo katika pendo, lazima pia tunapaswa kuiishi hiyo kweli. Maisha yetu ndiyo Biblia pekee ambayo baadhi ya watu huiona. Ndiyo maana Mtume Paulo anatuonya “tuuvue uongo, [na] tuseme kweli kila mtu na jirani yake; kwa maana tu viungo, kila mmoja kiungo cha wenzake” (Waefeso 4:25).

Ujasiri wa kweli katika imani hauji kikawaida tu, bali ni kitu kinachokua tunapoongezeka katika ujuzi wake Yeye ambaye ametuita katika nuru yake tukufu:

“Kueni katika neema, na katika kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo. Utukufu una yeye sasa na hata milele.” (2 Petro 3:18)

Author: Festus Patta

One Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *