Home 2021 September 16 “UTAUWA” Katika Siku Isiyomcha Mungu

“UTAUWA” Katika Siku Isiyomcha Mungu

“UTAUWA” Katika Siku Isiyomcha Mungu

Ni jambo la kushangaza kwamba maneno “utauwa” na “uchaji” yanapatikana kwa nadra katika maandishi ya Paulo hadi tunapozifika Nyaraka zake za Kichungaji, zile nyaraka ambazo zinasema mengi juu ya nyakati mbaya na mazingira mabaya ya siku za mwisho.

Katika nyaraka zake kwa Timotheo tunasoma juu ya “nyakati za hatari” ambazo wakati huu wa neema zitakamilishwa, ambapo katika waraka wake kwa Tito tunasoma juu ya “waropokaji na wababaishaji, na wadanganyifu,” “waongo… waovu kama wanyama… walafi, wavivu,” ambao Shetani angewatumia kudhoofisha kazi na ushuhuda wa watumishi wa kweli wa Mungu.

“Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao” (2 Timotheo 3 : 1-5)

“Kwa maana kuna wengi wasiotii, wenye maneno yasiyo na maana, wadanganyaji, na hasa wale wa tohara, ambao yapasa wazibwe vinywa vyao. Hao wanapindua watu wa nyumba nzima, wakifundisha yasiyowapasa kwa ajili ya mapato ya aibu. Mtu wa kwao, nabii wao wenyewe, amesema, Wakrete ni waongo siku zote, hayawani wabaya, walafi wavivu” (Tito 1:10-11)

Kwa Timotheo na Tito, hawa vijana wa Mungu, Mtume Paulo alikuwa na mengi ya kusema juu ya utauwa, na hatupaswi kusahau kwamba maneno ya Mtume Paulo kwao pia ni Neno la Mungu kwetu, waumini wa Kristo, ambao kwa kweli wanaonekana kuishi katika siku za mwisho za kipindi cha neema, kilichozungukwa na wimbi kubwa la uovu linalozidi kuongezeka siku hadi siku na idadi inayozidi kuongezeka ya watu waovu, watu wasiomcha Mungu.

Hatumaanishi hapo kusema kwamba Mtume Paulo hajishughulishi na namna mbalimbali ya maisha ya Kikristo katika nyaraka zake zingine, bali badala yake tunaonyesha hapa kwamba katika Nyaraka hizi za Kichungaji Paulo anayapa kipaumbele maisha ya utauwa na ucha Mungu katikati ya uasi ulioongezeka na kutokumcha Mungu kulikozidi.

Mungu atusaidie, katika tabia na mwenendo wetu, ili tuweze kuonyesha “nguvu ya utauwa,” nguvu ya kiroho inayotokana na kumtanguliza Kristo katika mambo yetu vyote.

Kwa Utukufu Wake Kristo

Author: Festus Patta

3 Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *