Home 2021 July 25 Mitume 12 na Paulo

Mitume 12 na Paulo

Mitume 12 na Paulo

Katika kulinganisha huduma ya mitume kumi na mbili na ile ya Mtume Paulo, ni lazima tuchunguze kwa uangalifu sana, haya yafuatayo:

Wale kumi na wawili walichaguliwa na Kristo akiwa DUNIANI (Luka 6:13) wakati ambapo Paulo alichaguliwa baadaye na Kristo akiwa MBINGUNI (Matendo ya Mitume 9:3-5; 26:16).

Kabla ya uongofu wa Paulo wale kumi na wawili walikuwa wanamjua Kristo akiwa DUNIANI tu (1 Yohana 1:1). Hata wakati wa kupaa kwake mbinguni, walichokiona ni: “wingu likimpokea kutoka machoni pao” (Matendo 1:9) na hata wale malaika wawili waliojitokeza wakati wakiwa katika mshangao wao wa jambo hilo; waliwaambia hivi: “… Huyu Yesu aliyechukuliwa kutoka kwenu kwenda juu mbinguni…”; kana kwamba ‘alibebwa na upepo wa kisulisuli’. Lakini Paulo alimjua Kristo akiwa MBINGUNI tu, kwa kuwa hakuwahi kumuona akiwa hapa duniani (Matendo 26:16; 1 Wakorintho 15:8).

Wale kumi na wawili waliwakilisha taifa lao. Namba kumi na mbili haina uhusiano wowote ule na “Mwili mmoja” wa Kristo. Kama tujuavyo, Mzee Yakobo wa zamani; mwana wa Isaka, mjukuu wa Ibrahimu, “aliwazaa mababu kumi na wawili”, wazee wa Israeli (Matendo 7:8). Kutoka kwao yalitokea makabila kumi na mawili ya Israeli. Makabila haya yalikuwa na wakuu kumi na wawili juu yao, wakuu wa kabila za baba zao; nao ndio walikuwa vichwa vya wale maelfu ya Israeli (Hesabu 1:16). Hata wakati ule ambapo Israeli ilitawaliwa na wafalme, bado kulikuwa na wakuu hao kumi na wawili (maakida wa kabila za Israeli) – mmoja juu ya kila kabila (1 Mambo ya Nyakati 27:16-22). Hivyo, Bwana wetu, Yesu Kristo, alipokwenda kutangaza “injili ya ufalme” kwa Israeli, aliwachagua wakuu kumi na wawili kwa viti vya enzi kumi na viwili katika ufalme ujao (Mathayo 19:28).

Kwa upande mwingine, Paulo, kama mtume mmoja, anawakilisha “Mwili mmoja,” Kanisa la leo (Warumi 12:5; 1 Wakorintho 12:13; Waefeso 4:4). Kwa sababu alikuwa vyote, mzaliwa wa Kiebrania na mzaliwa wa Kirumi, aliwakilisha wote, Wayahudi na Wayunani walioamini, “waliopatanishwa… na Mungu katika mwili mmoja kwa msalaba” (Waefeso 2:13-18).

Wale kumi na wawili walitumwa kutangaza ufalme wa Kristo (ufalme wa mbinguni) kuwa “umekaribia” (Mathayo 10:7), na baadaye ‘kutoa ofa’ ya kuanzishwa kwake duniani (Matendo 3:19-26). Lakini Paulo alitumwa kutangaza “injili ya neema ya Mungu” (Matendo 20:24), wakati kuanzishwa kwa ufalme ‘kukiwa kumeshikiliwa’.

Huduma ya wale mitume kumi na wawili ilijengeka juu ya ahadi za agano (Isaya 60:1-3; Luka 1:70-79; Matendo 3:22-26). Huduma ya Paulo haikujengeka juu ya ahadi za agano, bali ilijengeka juu ya neema ya Mungu tu kupitia Kristo (Warumi 3:21-28; 5:20-21; Waefeso 1:6-7; 2:7; n.k).

Kwa Utukufu Wake Kristo

Author: Festus Patta

One Comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *