Je Biblia Kweli ni Neno la Mungu
Jibu letu katika swali hili halitagusia tu mtazamo wetu juu ya Biblia na umuhimu wake maishani mwetu bali pia hatimaye litakuwa na mguso wa milele maishani mwako. Kama Biblia kweli ni neno la Mungu, basi natulifurahie, tulisome, tulitii na kuliamini. Kupewa kwetu Biblia na Mungu ni kithibitisho cha kuwa Mungu anatupenda. Neno ufunuo lina maana ya kuwa Mungu aliwasiliana na mwanadamu kumjuza jinsi alivyo na ni kwa jinsi gani tunaweza kupata ushirika mwema naye. Haya ni mambo ambayo tusingeweza kuyajua kama Mungu asingeyafunua kwetu kupitia Biblia. Ijapokuwa ufunuo wa Mungu katika Biblia umetolewa kwa mfululizo ndani ya takriban miaka 1,500 umehifadhi kila kitu ambacho mwanadamu anakihitaji ili aweze kumjua Mungu na kuwa na ushirika mwema naye.
Kama Biblia ni neno la Mungu kweli, basi ndiyo mamlaka ya mwisho katika mambo ya Imani ya Kikristo. Swali ambalo ni muhimu tujiulize ni kwamba tunawezaje kujua kuwa Bibilia ni neno la Mungu wala si kitabu tu kama vitabu vingine? Ni kitu gani maaluum ndani ya Biblia ambacho huifanya Biblia iwe kitabu maalum dhidi ya vitabu vingine vya dini? Je, kuna ushahidi kuwa Biblia ni neno la Mungu kweli? Hayo ni baadhi ya maswali ambayo yanahitaji kuangaliwa kama tunahitaji kujua kweli Biblia ni neon la Mungu, lilitoka kwake na lenye kujitosheleza katika mambo yote ya kiimani. Hakuwezi kuwa na mashaka kwamba Biblia ni neno la Mungu. Haya yanapatikana katika sura mbalimbali kama vile 2 Timotheo 3:15-17, inayosema, “na ya kuwa tangu utotoni mmeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuheshimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu. Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila kazi njema”.
Ili tuyajibu maswali haya kwa usahihi, lazima tutazame ushahidi wa ndani na wa nje yakuwa kweli Biblia ni neno la Mungu. Ushahidi wa ndani ya Biblia ni yale maandiko ambayo yanaelezea kuhusu chanzo cha kuwako kwake. Ushahdi wa kwanza ni katika ule umoja wake, yaani jinsi maandiko yake yanavyopatana. Ingawa Biblia ina vitabu sitini na sita vilivyoandikwa katika mabara matatu kwa lugha tatu tofauti ndani ya takriban miaka 1,500 na waandishi zaidi ya 40 (waliotoka katika taaluma mbalimbali), Biblia inabaki ni kitabu chenye kuhifadhi umoja kutoka mwanzo mpaka mwisho bila kujipinga chenyewe. Hali hii ni ya muhimu sana ukilinganisha na vitabu vyengine na inathibitisha kuweko kwa sauti ya Mungu ikinakiliwa na wanadamu.
Jambo lingine katika ushahidi wa ndani, linapatikana katika unabii ulioorodheshwa ndani ya vitabu mbalimbali za Biblia. Humu tunapata unabii juu ya mataifa kama vile Israeli, unabii wa miji fulani, unabii wa maisha ya wanadamu na hata wa kuja kwake Masihi mwokozi , si mwokozi wa Israeli tu balikwa wote watakao mwamini. Kinyume cha unabii unaopatikana katika vitabu vyengine, unabii wa kibiblia unatimia, kuna nabii zaidi ya mia tatu kuhusu Yesu Kristo katika Agano la kale pekee. Haikutabiriwa tu atazaliwa wapi na atakuwa wa jamii gani, lakini pia ya kuwa angekufa na kufufuka siku ya tatu. Hakuna njia mwafaka ya kuelezea ni kwa uwezo gani unabii huu ulitimizwa ispokuwa kukiri ni kwa uwezo wa Mungu. Hakuna kitabu kingine cha dini chenye unabii uliokamilika kama unabii uliotolewa kwenye Biblia.
Ushahidi wa tatu unapatikana katika uweza na mamlaka ya Biblia, hili si jambo dogo la kupuuzwa. Biblia ina mamlaka kuliko vitabu vyovyote vyengine, uwezo huu unaonekana katika maisha ya watu wengi wasiohesabika ambao wameweza kubadilishwa maisha yao kwa kusoma Biblia. Wenye kutumia mihadarati wameponywa, wahalifu sugu pia wamebadilishwa, wenye dhambi wamekaripiwa, wenye chuki wamebadilishwa na kuwa na upendo kwa kuisoma Biblia. Biblia ina uwezo wa kubadilisha maisha ya mtu kwa kuwa ni neno la Mungu. Mbali na ushahidi wa ndani ya Biblia yenyewe, kuna ushahidi wa nje ya Biblia unaothibitisha kuwa Biblia kweli ni neno la Mungu. Umakini wa historia kama inavyoelezewa katika Biblia ni ushahidi pia. Kupitia watafiti wa mabaki ya vitu vya kale na vitabu vyengine vilivyoandikwa, matukio ya kihistoria katika Biblia yamehakikishwa mara kwa mara kuwa ya kweli. Watafiti hao pamoja na majarida wanayoyaandika husema ya kwamba Biblia ndicho kitabu chenye kuongoza katika historia sahihi ya maeneo mbalimbali. Jinsi Biblia ilivyohifadhi historia sahihi ya vizazi mbalimbali ni uthibitisho ya kuwa ni kitabu cha kweli hasa katika kushughulikia maswala ya dini na mafundisho yake. Hili pia huthibitisha ya kuwa hili kweli ni neno la Mungu.
Jambo lingine linahusu heshima ya waandishi wa habari hizi za Biblia. Mungu aliwatumia watu wa tabaka mbalimbali kuandika habari hizi. Tukichunguza maisha ya watu hawa kwamba walikuwa tayari hata kufa kwa ajili ya uaminifu wao kwa Mungu kwa ajili ya yale waliyoyaamini; inathibitisha kuwa, watu hawa wanyonge na waaminifu walikuwa na uhakika kwamba Mungu kweli alikuwa amezungumza nao. Kwa mfano, wale waliondika Agano Jipya na mamia ya waumini wengine (1 Wakorintho 15:6) walijua ukweli wa ujumbe wao kwa kuwa walikuwa wamemuona na kushirikiana na Yesu Kristo baada ya kufa. Mabadiliko ya kumuona Kristo aliyefufuka yalipokewa na uzito mkuu na watu hawa. Walibadilika kutoka kwa waoga wa kujificha na kuwa watu ambao hawaogopi kufa kwa ajili ya ujumbe wa Mungu uliokuwa umefunuliwa kwao. Maisha yao na vifo vyao vinathibitisha ya kwamba kweli Biblia ni Neno la Mungu.
Ushahidi mwingine ni katika ile hali ya kutokuharibiwa kwa Biblia. Kwa sababu ya umuhimu wake na kwamba ni neno la Mungu, Biblia imepitia mapambano ya hatari mengi katika majaribio ya kutaka kuiharibu na kuipoteza Biblia katika historia yake kuliko kitabu chochote kingine tangu nyakati za watawala wa kirumi na kwa madikteta wa kikomiunisti na wale wasioamini kama kuna Mungu wanaoishi siku hizi, Pamoja na hayo yote Biblia imedhibiti hali yake na kudumu zaidi ya wapinzani wake. Hata sasa, ndicho kitabu kinachochapishwa kwa wingi zaidi duniani. Vizazi vyote na nyakati mbalimbali duniani kote wapinzani wamekuwa wakipuuza Biblia na kusema ni hadithi tu za watu lakini watafiti wa kihistoria wamezidi kuthibitisha ya kuwa Biblia ni kitabu cha kweli. Pia wapinzani wake wameshutumu mafundisho yake kuwa ni ya kijadi na yaliyopitwa na wakati lakini wema wake na mfumo wake wa kisheria umekubalika katika jamii na mila mbalimbali kote duniani. Biblia inaendelea kushambuliwa na wana sayansi, saikologia, na vyama vya kisiasa na bado Biblia inabaki na umuhimu ule ule uliokuwa nao wakati ikiandikwa. Ni kitabu kilichobadilisha maisha na tamaduni mbalimbali kwa muda wote wa miaka zaidi ya 2000 iliyopita. Haijalishi wapinzani wake wanapambana kivipi, Biblia inabaki kuwa ni kitabu chenye nguvu, na cha kweli na chenye umuhimu sawa na ule kilichokuwa nao kabla ya kupigwa vita. Kuhifadhika kwa hali yake ya asili hata baada ya mashambulizi haya yote ni ishara ya kuwa Biblia ni neno la Mungu. Isitushangaze ile hali ya kuwa Biblia inapigwa vita na kuibuka bado mshindi bila madhara yoyote. Kumbuka Yesu mwenyewe alisema, Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe (Marko 13:31). Ama hakika, Biblia kweli ni Neno la Mungu.
Leave a Reply