Home 2024 May 10 KUSUDI LA MUNGU KATIKA KIZUIZI CHA SHETANI

KUSUDI LA MUNGU KATIKA KIZUIZI CHA SHETANI

KUSUDI LA MUNGU KATIKA KIZUIZI CHA SHETANI

“Kwa hiyo tulitaka kuja kwenu, naam, mimi Paulo, mara ya kwanza, na mara ya pili, na Shetani akatuzuia” (1 Wathesalonike 2:18).

Mungu ana mpango katika maisha ya kila mmoja wetu, mpango ambao ni kwa faida yetu na utukufu wake. Hatupaswi kusahau, hata hivyo, kwamba Shetani naye pia ana mpango kwa ajili ya maisha ya mwamini pia. Kusudi la mpango wake ni kuharibu maisha yetu na ushuhuda wetu kwa Kristo kupitia dhambi, imani potofu, na maamuzi mabaya.

Kutajwa kwa “hila za Shetani” na Mtume Paulo katika Waefeso 6:11 kunatufundisha kwamba Shetani ana mikakati, mbinu, na njama ya kutufanya tuanguke au tushindwe katika vita vya kiroho. Tunajua kwamba, Shetani hawezi kukunyang’anya wokovu wako (Wakolosai 3:3); ingawa anaweza kuharibu ushuhuda wako. Kama ilivyo kwa mwizi, anaweza pia kukuibia furaha yako katika Kristo na uhakikisho wako wa wokovu.

Baada ya kuanzisha Kanisa la Thesalonike na kuondoka, Mtume Paulo alijaribu “mara moja na zaidi” kujiaunganisha tena na Kanisa hilo kwa kulitembelea, lakini haikufanikiwa. Sababu, iliyoandikwa na Mtume Paulo, ya kushindwa kwake huko ilikuwa ni kwamba ‘Shetani aliwazuia’. Neno la Kiyunani lililotafsiriwa “kuzuiliwa” linatumika kuonyesha kizuizi kinachoifanya barabara isipitike. Katika muktadha wa ki-riadha, neno hilo linamaanisha kumkata (kumkwatua) mtu wakati wa mbio. Katika muktadha wa kijeshi, neno hilo lilirejelea kukata daraja (mtaro) mbele ya jeshi linalosonga mbele ili kulizuia lisiweze kusonga mbele na kumkaribia adui. Shetani naye, anafanya jambo lilo hilo katika maisha yetu ya Kikristo: anatuzuilia njia, anatukwatua katikati ya hatua zetu ili kutukwaza, na au kuyazuia maendeleo yetu ya kiroho.

Hatujui ni nini hasa ambacho Shetani alikifanya ili kumzuia Mtume Paulo asiweze kurudi tena Thesalonike, lakini tunachokijua ni kwamba Mtume Paulo alikihusisha kizuizi hicho, moja kwa moja na Shetani mwenyewe. Lakini, hata hivyo, tunaona sasa jinsi kizuizi hicho cha Shetani kilivyokuwa sehemu ya usimamizi wa Mungu kwa maisha ya Mtume Paulo. Mungu aliruhusu na kuutumia upinzani huo wa Shetani na kuleta mema kutoka kwenye kizuizi hiki ambacho Mtume Paulo alikiona kuwa ni kibaya. Ni kama alivyofanya kwenye Msalaba, Mungu alitimiza makusudi yake ya ukombozi kupitia Msalaba huo, huku akimtumia shetani kufanya hivyo!

Tokeo la kushindwa kwa Mtume Paulo kwenda Thesalonike lilikuwa ni kuandikwa kwa barua, barua ambayo ilikuja kuwa sehemu ya Biblia yetu (Waraka wa Kwanza kwa Wathesalonike). Barua hii, kwa upande wake, imetokea kuwa utukufu kwa Mungu na, kwa takribani miaka 2000 iliyopita, watu wengi wasiohesabika wamefaidika na Waraka huu wa Kwanza wa Mtume Paulo kwa Wathesalonike na watu hao wamebarikiwa na kweli zake za kimungu zilizo nyingi; Moja yake ikiwa ni – tumaini letu lenye baraka la Unyakuo (4:13-18).

Ni kwa sababu tu Mtume Paulo alikabiliwa na kizuizi cha kishetani maishani mwake kwamba leo tuna ‘1 Wathesalonike’. Tunapaswa kukumbuka jambo hilo wakati wowote tunapokabiliwa na njia iliyofungwa au kupata kizuizi maishani mwetu ambacho tunaona kuwa ni kibaya, kwani Mungu anaweza kufanya kazi yake yeye mwenyewe ili kuleta kitu kizuri kutokana na kizuizi au kikwazo hicho kwa AJILI YA UTUKUFU WAKE.

Utukufu una Yeye KRISTO Milele na Milele AMINA

Author: Festus Patta

2 Comments

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *