Home 2024 September 05 MACHO YA BWANA!

MACHO YA BWANA!

MACHO YA BWANA!

“Macho ya Bwana hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake” (2 Nyakati 16:9)

Maana ya kifungu hiki maarufu cha Maandiko iko wazi, na ukweli wake umedhihirishwa mara elfu nyingi. Mungu, wakati wote, anatafuta wanadamu ambao Anaweza kuwabariki na kuwatumia katika kutimiza makusudi Yake, ingawa swali linabaki kuwa ni kwa ajili ya nani, na kwa kupitia nani, Mungu huyatimiza makusudi Yake?

Mungu, hahitaji ‘majitu’ yenye ushawishi mkubwa duniani, kwa maana Anasema katika Zekaria 4:6: “Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi.” Mungu, hawahitaji wasomi wakuu wa ulimwengu huu, kwani Bwana wetu, alipokuwa hapa duniani, alithibitisha hilo kwa kusema kuwa: “mambo haya uliwaficha wenye hekima na akili, ukawafunulia watoto wachanga. Naam, Baba, kwa kuwa ndivyo ilivyopendeza mbele zako” (Mathayo 11:25-26). Na ndio maana, Mtume Paulo anatangaza, katika 1 Wakorintho 3:19, kwamba: “Hekima ya dunia hii ni upuzi mbele za Mungu. Kwa maana imeandikwa, Yeye ndiye awanasaye wenye hekima katika hila yao.”

Hakika, si juu ya wakuu wa ulimwengu huu, ambapo Mungu hutoa baraka na uwezo Wake; bali ni juu ya Muumini mnyenyekevu ambaye moyo wake uko safi mbele zake. Hivyo, kwa uvuvio wa Roho Mtakatifu, Mtume Paulo aliwaandikia ndugu wa Korintho ya kale, wale waliokuwa wamemwamini Kristo kama Mwokozi wao, akiwaambia:

“Maana, ndugu zangu, angalieni mwito wenu, ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheo walioitwa; bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima; tena Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu; tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia na vilivyodharauliwa, naam, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko; mwenye mwili awaye yote asije akajisifu mbele za Mungu.” (1 Wakorintho 26-29)

Utukufu una Yeye KRISTO YESU Milele na Milele AMINA

Author: Festus Patta

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *